Drop Down MenusCSS Drop Down MenuPure CSS Dropdown Menu

Thursday, August 13, 2015

Majina rasmi ya wagombea Ubunge CCM 2015 yatajwa


Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) leo kimetangaza majina ya wagombea ubunge, ubunge viti maalum, uwakilishi na uwakilishi viti maalum ambapo baadhi ya wagombea walioshinda kwenye kura za maoni wametupwa nje na kuchukuliwa mshindi wa tatu.
 
Akizungumza leo na waandishi wa habari kwenye ofisi za makao makuu ya CCM mjini Dodoma, Katibu wa Itikadi na Uenezi Nape Nnauye amesema kuwa kuna baadhi ya majimbo ambayo yamelazimika kurudia kupiga kura za maoni na mengine kuhesabu upya kura zilizopigwa baada ya kujitokeza malalamiko kwa wagombea.
 
Amesema kuna baadhi ya majimbo ambayo wamelazimika kumchukua mshindi wa tatu kwenye kura za maoni na kuwaacha walioshinda nafasi ya kwanza na ya pili ili kumaliza migogoro iliyokuwepo.
 
Ameyataja majimbo 11 ambayo yatarudia uchaguzi wa kura za maoni kuwa ni Ukonga, Kiteto, Chilonwa, Kilolo, Njombe Kusini, Makete, Namtumbo, Rufiji, Mbinga Vijijini, Busega na Singida Mashariki.
 
Aidha Nnauye amesema kuwa uchaguzi wa viti maalum kupitia umoja wa wanawake Tanzania (UWT) yamepitishwa kama yalivyotoka mikoani ambapo ni mkoa mmoja tu wa Dar es Salaam ambao NEC imetengua ushindi wa mshindi wa kwanza, Angela Kiziga ambaye ni mbunge wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na badala yake aliyeshika nafasi ya pili na ya tatu ndiyo waliopitishwa katika ubunge wa viti maalum.
 
Waliopitishwa na Halmashauri Kuu ya CCM kwenye ubunge wa viti maalum mkoa wa Dar es Salaam ni Mariam Kisangi aliyekuwa mshindi wa pili na Janeth Masaburi aliyekuwa mshindi wa tatu.

No comments:

Post a Comment